NHIF SHINYANGA YAWAASA WANANCHI KUJIUNGA NA BIMA YA AFYA KUPUNGUZA GHARAMA ZA MATIBABU


Meneja wa NHIF) Mkoa wa Shinyanga Isaac Katenda

Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Shinyanga, Isaac Katenda, amewahimiza wananchi kujiunga na bima ya afya ili kuepuka gharama kubwa za matibabu.

Katenda amesema wananchi wanapaswa kuondokana na dhana ya kutafuta bima ya afya pale tu wanapokuwa na mgonjwa anayehitaji matibabu ya muda mrefu, na badala yake wajenge utamaduni wa kujiunga mapema na bima hiyo ili kuwa na uhakika wa kupata nafuu ya huduma za afya kwa familia zao.

Amesema NHIF inaendelea kupokea wanachama wapya wakati Serikali ikiendelea kukamilisha mchakato wa utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote, huku akibainisha kuwa mwongozo zaidi utatolewa kwa wale watakaokutwa wamejiunga na NHIF mara baada ya mchakato huo kukamilika.

Katenda ameeleza kuwa, NHIF kwa sasa inatoa vifurushi mbalimbali kulingana na mahitaji ya wananchi ambavyo vimegawanywa katika makundi matano ya Tarangire, Ngorongoro afya, Mikumi, Serengeti na Tanzanite ambavyo vinaambatana na punguzo kubwa kwa wale wanaojiunga kifamilia.

Katenda amesema huduma za NHIF zinapatikana kwenye zaidi vituo zaidi ya 10,000 vya kutolea huduma za afya nchini, kuanzia ngazi ya zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, Hospitali za rufaa za mikoa na kanda hadi hospitali za taifa.

Amefafanua kuwa vifurushi vyote vinajumuisha huduma muhimu za vipimo na dawa, huku tofauti kubwa ikiwa katika wigo wa huduma na mahitaji maalumu ya wanachama.

Pia amewataka wananchi kujenga tabia ya kutembelea ofisi za NHIF zilizopo karibu yao ili kupata elimu sahihi kuhusu huduma za bima ya afya, masharti ya kujiunga na vifurushi vinavyowafaa kulingana na mahitaji yao.

Amesema hatua hiyo itasaidia kuondoa upotoshaji wa taarifa na kuwawezesha wananchi kufanya maamuzi sahihi na kwamba bima ya afya si gharama ikilinganishwa na utaratibu wa kawaida wa matibabu, bali ni uwekezaji muhimu unaowasaidia kukabiliana na changamoto za kiafya bila kuathiri hali zao za kiuchumi.

Kuhusu utekelezaji wa Bima ya Afya kwa wote, Katenda amesema kwa sasa huduma hiyo imeanza kutolewa kwa kaya zisizo na uwezo zinazotambuliwa kupitia Mpango wa TASAF, ambapo Serikali inagharamia huduma hiyo kwa asilimia 100.

Ameongeza kuwa makundi mengine ya wananchi yataanza kunufaika na Bima ya afya kwa wote mara tu mchakato utakapokamilika.

 

Post a Comment

0 Comments