Akizungumza
wakati wa ziara ya kutambulisha huduma za chuo hicho katika mikoa ya Kanda ya
Ziwa, ikiwemo Shinyanga, Afisa Masoko wa KIUT, Gaudence Tracy, alisema chuo
hicho kinaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu kozi mbalimbali zinazotolewa
kuanzia ngazi ya Cheti, Stashahada, Shahada, Shahada ya Uzamili hadi Shahada ya
Uzamivu (PhD), pamoja na fursa za ufadhili zinazopatikana.
Alisema ufadhili huo unalenga zaidi kozi za Sayansi ya Jamii, ambapo wanafunzi wanaweza kupata punguzo la ada hadi asilimia 50 kulingana na sifa na masharti yaliyowekwa. Aidha, kwa wanafunzi wanaopata mikopo ya elimu ya juu kutoka serikalini isiyofikia asilimia 100 ya mahitaji yao, KIUT itasaidia kugharamia sehemu ya gharama inayobaki ili kuwawezesha kuendelea na masomo yao bila vikwazo vya kifedha.
“Lengo letu
ni kuhakikisha kwamba kila mtu mwenye sifa za kujiunga na elimu ya juu anapata
nafasi hiyo bila kuzuiwa na changamoto za kipato. Tunaamini elimu ni nyenzo
muhimu ya maendeleo ya mtu binafsi na taifa kwa ujumla,” alisema Tracy.
Aliongeza
kuwa taarifa zote kuhusu udahili, kozi zinazotolewa na taratibu za kujiunga na
chuo hicho zinapatikana kupitia tovuti rasmi ya KIUT ya www.kiut.ac.tz
KIUT ni tawi
la Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala kilichoanzishwa nchini Uganda mwaka
2001. Nchini Tanzania, taasisi hiyo ilianza mwaka 2008 kama chuo kishiriki cha
Dar es Salaam (KIU-DCC) chini ya Kampala International University.
Mnamo
Januari 15, 2011, chuo hicho kilipata usajili wa muda kutoka Tume ya chuo kikuu
Tanzania (TCU), kabla ya kupewa usajili kamili tarehe 27 Septemba 2012.
Baadaye, tarehe 17 Julai 2017, TCU ilikipa hadhi ya kuwa chuo kikuu kamili kwa
jina la Kampala International University in Tanzania (KIUT).
Kutokana na
ubora wa huduma za elimu zinazotolewa, tarehe 2 Agosti 2022 chuo hicho
kilitunukiwa cheti cha ithibati, hatua iliyothibitisha kukidhi viwango
vinavyohitajika katika utoaji wa elimu ya juu nchini.
Kwa sasa,
KIUT ambacho kwa Tanzania kiko eneo la Gongo la Mboto Jijini Dar es salaam, ni
miongoni mwa vyuo vikuu vinavyotoa programu mbalimbali zinazolenga kukidhi
mahitaji ya maendeleo ya jamii katika nyanja tofauti, zikiwemo Sayansi za
Jamii, Uhandisi, Kilimo, Sheria, Sayansi za Afya, Biashara, Elimu pamoja na
Sayansi na Teknolojia.


0 Comments