Wito huo umetolewa Agosti 7, 2026, na Mkurugenzi Msaidizi
wa Rasilimali Watu wa Wizara ya Afya, Bi. Amisa Mwakawago, wakati akifunga
Maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani 2026 na kuzindua chumba maalum cha
unyonyeshaji katika Ofisi za Wizara ya Afya, Mtumba, jijini Dodoma.
Maadhimisho hayo yamefanyika chini ya kaulimbiu “Mwanzo
Imara wa Maisha ya Mtoto Huanza na Maziwa ya Mama.”
Bi. Mwakawago amesema uzinduzi wa chumba hicho unaonesha
dhamira ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwawezesha wanawake
kuendelea kunyonyesha watoto wao baada ya kurejea kazini.
Amesema unyonyeshaji wa maziwa ya mama pekee kwa miezi sita
ya kwanza ni miongoni mwa afua zenye matokeo makubwa katika kuokoa maisha ya
watoto, kuimarisha kinga ya mwili, kuboresha lishe na kuchangia ukuaji na
maendeleo ya ubongo.
Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali, Dkt. Eliud
Eliakimu, amesema mafanikio katika unyonyeshaji yanahitaji ushirikiano wa
familia, jamii, watoa huduma za afya, waajiri na wadau wa maendeleo.
Amesisitiza umuhimu wa kumwezesha mama kuanza kunyonyesha
mapema, kumpa mtoto maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya kwanza na kuendelea
kunyonyesha hadi mtoto atimize miaka miwili au zaidi, sambamba na kumpatia
lishe bora ya nyongeza.
Dkt. Eliakimu pia amehimiza kuunganishwa kwa huduma za
unyonyeshaji na huduma za malezi na makuzi ya awali ya mtoto, ikiwemo kuwapatia
wazazi na walezi elimu kuhusu malezi yenye upendo, mawasiliano chanya na
matumizi ya michezo katika kujifunza.
Amesema hatua hizo ni muhimu katika kujenga msingi imara wa
ukuaji na maendeleo ya mtoto.
Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Kinga, Sehemu ya
Epidemiolojia, Dkt. Vida Mmbaga, amezitaka taasisi za umma na binafsi kuanzisha
na kuimarisha vyumba vya unyonyeshaji pamoja na kuweka sera rafiki kwa wazazi
mahali pa kazi.
Amesema hatua hiyo itasaidia kulinda haki ya mtoto kupata
maziwa ya mama, huku ikimuwezesha mama kutekeleza majukumu yake ya kikazi kwa
ufanisi.
Dkt. Mmbaga amesisitiza kuwa uwekezaji katika unyonyeshaji
ni sehemu muhimu ya uwekezaji katika afya ya jamii na maendeleo ya Taifa.
Imeandikwa na Andrea Kadege, Wizara Afya – Dodoma

0 Comments