Mkurugenzi Mkuu wa WHO Tedros Adhanom Ghebreyesus ametoa
wito wa kuongeza kasi ya kukabiliana na mlipuko huo na kusema kwamba Ebola
inaweza kudhibitiwa.
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inakabiliwa na hatua
nyingine ya kutisha katika mlipuko wake wa Ebola, baada ya idadi ya visa
vilivyothibitishwa kuvuka 4,000 kwa mara ya kwanza, huku kukiwa na hofu mpya
kwamba virusi hivyo vinaweza kusogea karibu na mji mkuu Kinshasa.
Takwimu za hivi karibuni za taasisi ya afya ya umma
ya DRC zinaonyesha visa 4,053
vimethibitishwa, na watu 1,850 wamefariki dunia.
Huu ni mlipuko wa pili kwa ukubwa zaidi kuwahi kurekodiwa
duniani, baada ya ule wa Afrika Magharibi wa mwaka 2014 hadi 2016 uliokuwa na
zaidi ya visa 28,000.
Mlipuko wa sasa umeenea katika majimbo matano ya Ituri,
Kivu Kaskazini, Kivu Kusini, Haut-Uele na Tshopo, huku Ituri ndiyo kitovu
kikuu.
Lakini wasiwasi umeongezeka zaidi baada ya mtu anayeshukiwa
kuwa na Ebola kufariki ndani ya boti
iliyokuwa ikielekea Kinshasa kutoka Tshopo.
Mamlaka ziliifuatilia boti hiyo na kuizuia umbali wa
kilomita 65 kutoka Kinshasa, mji wenye wakazi karibu milioni 17.
Maabara inayohamishika imepelekwa eneo hilo kuwapima abiria wote, huku boti ikiendelea kutengwa.


0 Comments