NGOs ZASHAURIWA KUBUNI NJIA MBADALA KUPATA MAPATO YA KUENDELEZA MIRADI


Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga Bw.David Lyamongi


Viongozi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) mkoani 
Shinyanga, wameshauriwa kubuni vyanzo mbadala vya mapato, ili kuendeleza miradi wanayoianzisha, badala ya kutegemea wafadhili wa nje pekee.

Ushauri huo umetolewa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi, wakati akifungua Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali mkoani hapa, lililofanyika katika Ukumbi wa Mkoa mjini Shinyanga.

Lyamongi, ambaye pia ni Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia Raslimali Watu na Utawala, amesema hatua hiyo itasaidia mashirika hayo kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali, hata pale wafadhili wanapositisha ufadhili.

Amesema mashirika mengi yamekuwa yakishindwa kuendeleza miradi yaliyoianzisha kutokana na utegemezi mkubwa wa ufadhili kutoka nje ya nchi, ikiwemo mataifa ya Ulaya, wakati wafadhili hao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali, zikiwemo kuweka masharti mapya na magumu au kusitisha kabisa ufadhili.

Kutokana na hali hiyo, Lyamongi ameyataka mashirika hayo kuanzisha shughuli za uzalishaji zinazoendana na malengo yao, ili kupata mapato ya kusaidia gharama za uendeshaji na utekelezaji wa miradi.

Aidha, ameyapongeza Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa mchango mkubwa yanayoutoa katika maendeleo ya nchi, akisema yamekuwa wadau muhimu wa Serikali kwa miaka mingi katika maeneo mbalimbali, ikiwemo katika Sekta ya afya, elimu, uwezeshaji wa wanawake na vijana, mazingira, haki za binadamu, ustawi wa jamii, kupunguza umaskini na kuongeza fursa za kiuchumi.

Ameyataka mashirika hayo kuhakikisha mipango na utekelezaji wa shughuli zao unaendana na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050, inayolenga kuimarisha ustawi na maendeleo ya taifa.

Hata hivyo, washiriki wa jukwaa hilo waliomba ufafanuzi kuhusu ushauri wa NGOs kuanzisha shughuli za uzalishaji kwa ajili ya kupata mapato, wakitaka kujua iwapo hatua hiyo haitaweza kutafsiriwa kuwa mashirika hayo yameanza kufanya biashara na hivyo kudaiwa kodi, kinyume na malengo ya kuanzishwa kwake.

Mkurugenzi Mtendji wa Shirika la THUBUTU AFRICA INITIATIVES Bw. Jonathan Kifunda akiomba ufafanuzi kwa TRA kuhusu NGOs kuanzisha shughuli za uzalishaji 

Akifafanua suala hilo, Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Focus Magobe, amesema shughuli hizo hazipaswi kuwa na lengo la kibiashara, bali zijikite katika kusaidia mashirika kuendeleza shughuli zao.

Ametolea mfano wa shughuli za kilimo cha mazao mbalimbali yanayoisaidia jamii kuingiza kipato ambazo hazitozwi kodi, akisema uzalishaji wake unahesabika kuwa uko kwa ajili ya kujikimu, na hauchukuliwi  kama wenye malengo ya kibiashara.

 Afisa Mkuu Msimamizi wa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Focus Magobe

Wakati huohuo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mkoa wa Shinyanga, Rehema Edson, ameyataka mashirika yote yanayofanya kazi mkoani hapa kuzingatia sheria na taratibu, ikiwemo kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa miradi kupitia mifumo iliyowekwa kwa wakati.
Afisa Maendeleo ya jamii wa mkoa wa Shinyanga Bi. Rehema Edson

Naye Mwakilishi wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NACONGO) Mkoa wa Shinyanga, Juma Bakari, amesema baraza hilo limechukua hatua mbalimbali za kukabiliana na changamoto za kiutendaji zinazoyakabili mashirika hayo.

Amesema miongoni mwa hatua hizo ni kuyakutanisha mashirika na mamlaka za Serikali, ikiwemo TRA, ili kupata maelekezo kuhusu utekelezaji wa majukumu yao. 

Aidha, amesema NACONGO inaendelea na mchakato wa kuanzisha mitandao ya NGOs katika kila wilaya.

Mwakilishi wa Baraza la Taifa la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NACONGO) Mkoa wa Shinyanga, Juma Bakari

Kupitia jukwaa hilo, wadau mbalimbali walitoa elimu kuhusu masuala yanayohusu utekelezaji wa shughuli za NGOs.

TRA ilitoa elimu kuhusu umuhimu wa kuzingatia sheria na taratibu za kodi, huku Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ikieleza umuhimu wa uwazi, maadili na uzalendo katika utekelezaji wa shughuli za mashirika hayo.

Idara ya Uhamiaji ilitoa ufafanuzi kuhusu vigezo na taratibu za kupata vibali vya kuajiri raia wa kigeni, wakati Shirika la World Vision lilitoa mafunzo kuhusu mbinu za uandishi wa maandiko ya miradi (Project Proposals).

Kwa upande wake, Idara ya Maendeleo ya Jamii iliwasilisha taarifa kuhusu hali ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali mkoani Shinyanga na kueleza nafasi ya NGOs katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.

Kaulimbiu ya Jukwaa la Mwaka la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali mwaka huu inasema: “Fikra Mpya Kuhusu Uendelevu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali: Ubunifu, Ubia na Upatikanaji wa Rasilimali Fedha Kupitia Vyanzo vya Ndani.”

Mkuu wa Dawati la Elimu kwa Umma kutoka TAKUKURU mkoa wa Shinyanga Mohamed Doo akiwasilisha mada kwa washiriki
Kaimu Afisa uhamiaji wa Wilaya ya Shinyanga Elizabeth Godfrey Kaka akiwasilisha mada kwa washiriki
Meneja wa Kanda wa Shirika la World Vision Goodluck Nnko akiwasilisha mada kwa washiriki


 Afisa Matekelezo Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi ya jamii NSSF mkoa wa Shinyanga Bi. Hawa Godigodi akizungumza na washiriki

Wawakilishi wa NGOs wakitoa maoni yao kwenye jukwaa



PICHA ZA  MATUKIO MBALIMBALI KWENYE JUKWAA LA  NGOs MKOA WA SHINYANGA 2026

Post a Comment

0 Comments