Akifungua mafunzo ya siku moja yaliyoandaliwa na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kwa waandishi wa habari wa mkoa wa Shinyanga, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga, David Lyamongi, amesema waandishi wana wajibu wa kueleza kwa wananchi manufaa yanayotokana na miradi hiyo, pamoja na kuhamasisha jamii kutumia fursa za kiuchumi zinazopatikana kupitia miradi hiyo.
Amesema Serikali inaendelea kuweka mikakati ya kuendeleza sekta ya mafuta na gesi ili iwe sehemu muhimu ya kukuza uchumi wa Taifa na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050.
Ameongeza kuwa wananchi wanapaswa kutumia fursa
zinazotokana na miradi hiyo kuanzisha shughuli za kiuchumi zitakazowanufaisha ,
huku wakishirikiana na Serikali katika kulinda miundombinu ya miradi hiyo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na
Mawasiliano TPDC, Marie Msellemu, amesema mafunzo hayo ni sehemu ya mkakati wa
shirika kuimarisha ushirikiano na waandishi wa habari ili kuongeza uelewa wa
umma kuhusu sekta ya mafuta na gesi asilia.
Amesema gesi asilia ni hitaji la muhimu kwa sasa , kwa sababu inatakiwa kwenye matumizi mbalimbali ikiwemo majumbani, viwandani na kwenye vyombo vya usafiri, ambapoTPDC kwa kushirikiana na Serikali inaendelea na mikakati ya kuongeza wigo wa usambazaji wa nishati hiyo nchini.
Akizungumzia Bomba la EACOP, Kaimu Mratibu wa Mradi huo kutoka TPDC,
Jumanne Mohamed, amesema utekelezaji wake unazingatia masuala ya mazingira na
jamii, huku hatua mbalimbali zikichukuliwa kudhibiti athari zinazoweza kujitokeza.
Amesema mafuta yatarajiwa kuanza kuingizwa kwenye bomba
hilo ifikapo Januari 15, 2027 na kusafirishwa hadi kituo cha Chongoleani mkoani
Tanga, ambapo wabia wote ikiwemo Uganda na Tanzania watanufaikana mradi huo.
Kwa mujibu wa Jumanne, mradi huo umepita katika mikoa minane ya Tanzania ambayo ni Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida,Dodoma, Manyara na Tanga.
Kwa upande wa mkoa wa Shinyanga, bomba hilo linalotokea nchini Uganda, limepita Wilayani Kahama kwenye vijiji na mitaa 16, ambapo kaya 10 zilizoathiriwa na
utekelezaji wa mradi zimelipwa fidia, yenye thamani ya takribani Shilingi
bilioni 1.8.
Aidha, amebainisha kuwa, shughuli za utafutaji wa mafuta na
gesi zinazoendelea katika maeneo mbalimbali nchini, pia zinahusisha mkoa wa
Shinyanga katika Bonde la Eyasi-Wembere kwenye eneo la Wilaya ya
Kishapu.
Akizungumza kwa niaba ya wandishi wa Habari mara baada ya mufunzo hayo, Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Shinyanga, Greyson Kakuru, ameishukuru TPDC kwa kuwapa mafunzo ambayo yamewaongezea uelewa na uwezo wa kuripoti kwa usahihi kuhusu sekta ya mafuta na gesi, miradi ya kimkakati pamoja na fursa zinazotokana na sekta hiyo.
0 Comments