ASKARI WAWILI WAFARIKI KWA KUGONGWA NA GARI

 

Askari wawili wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani, wamefariki dunia baada ya kugongwa na gari wakati wakivuka katika kivuko cha waenda kwa miguu (Zebra), eneo la Mailimoja, Kibaha.

Tukio hilo lilitokea Agosti 25, 2026, majira ya saa 1:00 usiku katika Barabara Kuu ya Dar es Salaam–Morogoro.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Salim Morcase, amesema gari aina ya Toyota Noah lenye namba za usajili T 804 ERM, lililokuwa likitokea Dar es Salaam kuelekea Mlandizi, liliwagonga askari hao baada ya dereva kulipita gari lililokuwa limesimama kupisha waenda kwa miguu.

Amesema askari Izdory Michael alifariki papo hapo, huku askari wa kike, Rehema Magawa, akijeruhiwa na kukimbizwa Hospitali ya Rufaa ya Tumbi, ambako alifariki dunia asubuhi ya Agosti 26, 2026 kutokana na majeraha ya kichwa.

Kwa mujibu wa Kamanda Morcase, dereva alikimbia baada ya ajali, lakini Polisi kwa kushirikiana na wananchi walifanya msako na kulifanikiwa kulipata gari hilo majira ya saa 2:40 usiku eneo la Kwamfipa, Wilaya ya Kibaha, lilipokuwa limefichwa.

Miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Tumbi ikisubiri taratibu za kusafirishwa kwa ajili ya mazishi.

 SOURCE: IPP MEDIA

Post a Comment

0 Comments