DIWANI NDEMBEZI AELEZA MPANGO WA KUJENGWA KWA DARAJA LA MINZI

Diwani wa kata ya Ndembezi Pendo Sawa

Daraja la Minzi, linalowaunganisha wakazi wa mitaa ya Mbuyuni na Dome, Kata za Ndembezi katika Manispaa ya Shinyanga, linatarajiwa kujengwa upya, ili liweze kukidhi mahitaji ya watumiaji.

Akizungumza na wananchi wa Mtaa wa Dome kwenye mkutano  wa hadhara kwa lengo la kuwashukuru kwa kumchagua yeye na viongozi wengine chama cha mapinduzi (CCM), Diwani wa kata ya Ndembezi, Pendo Sawa, amesema mchakato wa ujenzi wa daraja hilo tayari umeanza baada ya hoja hiyo kupitishwa na Baraza la Madiwani la Manispaa ya Shinyanga, ambapo utekelezaji wa mradi huo utafanyika ndani ya mwaka huu wa fedha 2026/2027.

Amesema ujenzi wa daraja hilo unatarajiwa kugharimu takribani Shilingi milioni 123 mpaka kukamilika kwake, ambapo litawaondolea wananchi adha ya kufurika kwa maji kwenye eneo hilo hasa mvua zinaponyesha, hali inayowaletea usumbufu.

Katika hatua nyingine, Sawa amesema anaendelea kushirikiana na viongozi wengine, akiwemo Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Paschal Patrobas Katambi, katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili wananchi wa Kata ya Ndembezi.

Ametaja baadhi ya changamoto zilizotafutiwa ufumbuzi kuwa ni pamoja ujenzi wa Daraja la Butengwa, kufungua barabara za mitaa kwenye maeneo ya makazi mapya, kujenga mifereji ya maji pamoja na kushughulikia mgogoro wa ardhi kati ya wananchi wa mtaa wa Butengwa na kampuni ya CASEC ambao tayari umetatuliwa.

Sawa pia ameeleza kuhusu mchakato unaoendelea wa kuwarejesha wafanyabiashara wa Milunda kutoka Matanda kwenda eneo la Dome Garden, Kata ya Ndembezi, hatua ambayo ameitaja, inalenga kufungua na kuongeza fursa za kiuchumi na kibiashara kwa wananchi wa eneo hilo.


Post a Comment

0 Comments