HUDUMA ZA TIBA MAZOEZI HOSPITALI YA MANISPAA YA SHINYANGA ZABORESHWA

 

Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga imeboresha huduma za tiba mazoezi, hatua ambayo imewezesha wananchi kupata matibabu hayo kwa kiwango kinachotakiwa.

Akizungumza na Shinyanga One Media, Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Pierina Mwaluko, amesema maboresho hayo yanatokana na kuwepo kwa vifaa vya kisasa, vilivyotolewa na Wizara ya Afya, kupitia mpango wa Serikali wa kuboresha huduma za afya.

Amesema kwa sasa hospitali hiyo ina wataalamu wanne wa tiba mazoezi, ambapo mmoja yuko masomoni kwa ajili ya kuongeza ujuzi.

Mganga Mfawidhi wa hospitali ya Manispaa ya Shinyanga  Dkt. Pierina Mwaluko

Kwa mujibu wa Dkt. Mwaluko, huduma hizo zilianza kutolewa
 mwaka 2024, lakini zimeboreshwa zaidi mwaka 2025, baada ya hospitali hiyo kupokea vifaa vya kisasa.

Ameongeza kuwa,  huduma hiyo inatolewa kwa wananchi wote wakiwemo wagonjwa wa nje na waliolazwa Hospitalini hapo, kwa kuchangia gharama kidogo kulingana na miongozo iliyotolewa na wizara ya Afya.

Amesema upatikanaji wa huduma hiyo katika hospitali hiyo umesaidia kupunguza changamoto iliyokuwa ikiwakabili wananchi, ambao awali walilazimika kwenda katika hospitali binafsi jijini Mwanza au Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya kupata huduma hizo.

Kwa upande wake, mtaalamu wa tiba mazoezi katika hospitali hiyo, Elihuruma Keppa, amesema kwa sasa wanahudumia wagonjwa kati ya 10 na 20 kwa siku wenye mahitaji mbalimbali ya tiba mazoezi.

Amesema wagonjwa wanaofika kupata huduma hiyo ni pamoja waliopooza baadhi ya sehemu za miili kutokana na magonjwa mbalimbali kama kiharusi, waliojeruhiwa katika ajali, watoto wenye changamoto ya mfumo wa fahamu, wenye maumivu ya mgongo, shingo, nyonga na misuli na wenye ulemavu wa viungo,

Mtaalam wa mazoezi ya viungo katika Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga Elihuruma Keppa

Baadhi ya wananchi, wakiwemo wazee, wanaopata huduma za tiba mazoezi katika hospitali hiyo, wamesema huduma hiyo imewasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto za kiafya zilizokuwa zinawakabili.

Wameeleza kuwa upatikanaji wa huduma hiyo karibu na makazi yao umewaondolea usumbufu na gharama za kusafiri umbali mrefu kama ilivyokuwa awali.

Post a Comment

0 Comments