Kinachotia wasiwasi ni kwamba, baadhi ya nafasi hizo
hutangazwa bila kuweka wazi vigezo vya msingi vya ajira, huku waombaji
wakiahidiwa kuajiriwa au kupewa nafasi za kusimamia biashara ambazo wakati
mwingine hakuna uthibitisho wa kutosha kuhusu kampuni au shughuli hizo.
Baada ya kuvutiwa na matangazo hayo, waombaji huitwa katika ofisi ambazo mara nyingi ziko kwenye maeneo yaliyofichika.
Baadhi yao wanapofika
hukuta mazingira tofauti na matarajio yao, yakiwemo makundi ya vijana wenzao
wanaoishi pamoja katika mazingira yasiyofaa kiafya na kiusalama, huku
wakiendelea kuahidiwa kwamba taratibu za ajira zinaendelea.
Kadiri siku zinavyokwenda, baadhi yao huanza kuombwa fedha
kwa ajili ya chakula, malazi, usajili, vitambulisho, mafunzo na vifaa vya kazi.
Wengine hutakiwa kununua vifaa vya gharama kubwa, ikiwemo kompyuta mpakato, kwa
maelezo kwamba ni sehemu ya maandalizi kabla ya kuajiriwa.
Baadhi ya vijana waliowahi kuingia kwenye mtego huo, wanadai
kuzuiwa hata kuwasiliana kwa uhuru na ndugu zao au watu wengine wa nje, lakini
wakati huohuo hulazimishwa kuwapigia simu wazazi na ndugu zao wakiwa chini ya
uangalizi, ili kuwaomba fedha au kuwashawishi watu wengine kujiunga na mpango
huo.
Jambo hili linaweza kuwaumiza si vijana pekee, bali pia
familia zao. Baadhi ya wazazi, kwa kutarajia watoto wao kupata ajira,
hulazimika kutumia akiba au kuuza mali ili kupata fedha zinazohitajika. Mwisho
wa siku, iwapo ahadi ya ajira haitimizwi, familia hizo huachwa katika hasara
kubwa.
Ripoti za matukio ya aina hii zimekuwa zikijitokeza katika
maeneo mbalimbali nchini, jambo linaloonyesha umuhimu wa mamlaka husika
kulifuatilia kwa karibu na kuchukua hatua stahiki pale sheria zinapokiukwa.
Ni wakati sasa kwa mamlaka zinazohusika na ajira, biashara, ulinzi na usalama kushirikiana kufuatilia makundi na kampuni zinazotoa matangazo ya ajira yanayotia shaka.
Aidha, wananchi wanapaswa kuendelea kupewa
elimu kuhusu taratibu halali za kutafuta ajira na viashiria vya utapeli ili
wasipoteze fedha, muda na mali zao.
Kukosekana kwa hatua madhubuti dhidi ya vitendo hivi
kunatoa nafasi kwa waathirika kuongezeka. Mamlaka zisisubiri malalamiko
yaongezeke au madhara kuwa makubwa, zinapaswa kuchukua hatua mapema ili kulinda
vijana, familia zao na heshima ya soko la ajira nchini.

0 Comments