WAKUU WA TAASISI ZA UMMA FUATILIENI UTENDAJI WA WALIO CHINI YENU KUEPUKA MALALAMIKO

 

Baadhi ya taasisi za umma zimekuwa zikikabiliwa na malalamiko kutoka kwa wananchi kutokana na huduma kutotolewa kwa wakati na kwa ufanisi unaotarajiwa. 

Wakati mwingine, jambo linaloweza kukamilishwa kwa muda mfupi huwekewa mlolongo mrefu wa taratibu, hali inayowalazimisha wananchi kutumia muda na gharama zaidi. 

Katika mazingira kama hayo, baadhi yao hujikuta wakishawishika kutoa rushwa ili kupata huduma kwa haraka.

Ukifuatilia kwa undani, changamoto hii haiwezi kuhusishwa na Serikali au taasisi nzima, bali mara nyingi husababishwa na udhaifu katika usimamizi na uwajibikaji wa baadhi ya watendaji.

Wapo baadhi ya viongozi na wasimamizi ambao hawafuatilii kwa karibu namna watumishi walio chini yao wanavyotekeleza majukumu na kuwahudumia wananchi.

Ni muhimu kwa viongozi wa taasisi kujenga utamaduni wa kutembelea maeneo ya kutolea huduma, kuzungumza moja kwa moja na wananchi na kusikiliza maoni yao. 

Ufuatiliaji wa aina hiyo unaweza kusaidia kubaini mapema uzembe, ucheleweshaji usio wa lazima na vitendo vinavyoweza kuwafanya wananchi kuamini kuwa ili kupata huduma ni lazima watoe kitu.

Si jambo la kawaida kwa mwananchi kusafiri kutoka kijijini au eneo la mbali kwa ajili ya kupata huduma ambayo, kiuhalisia, inaweza kukamilishwa ndani ya siku moja, lakini akafika katika ofisi husika na kuambiwa arudi siku nyingine bila sababu ya msingi. Hali hiyo si tu kwamba inampotezea muda na kumwongezea gharama, bali pia inaweza kumjengea mtazamo hasi kuhusu huduma za Serikali.

Kwa hiyo, viongozi na wasimamizi wa taasisi za umma wanapaswa kuimarisha ufuatiliaji wa utendaji wa watumishi walio chini yao na kuhakikisha wananchi wanapata huduma kwa wakati, kwa haki na kwa heshima huku wale wanaobainika kuwa kikwazo kwa ufanisi wa taasisi waondolewe mara moja au wapangiwe majukumu mengine.

Wananchi wanapopata huduma bora, malalamiko hupungua, imani kwa taasisi huongezeka na taswira ya Serikali huimarika.

Ni muhimu kutambua kuwa, mara nyingi, kasoro za watumishi wachache zinaweza kuwafanya wananchi kuichukulia Serikali nzima kuwa haiwajali. Hivyo, uongozi madhubuti, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa watendaji ni sehemu muhimu ya kuhakikisha huduma za umma zinatolewa kwa ufanisi na si kwa matashi ya mtu kwa sababu tu yuko kwenye nafasi hiyo.

Post a Comment

0 Comments