TRA YAENDELEA KUTOA UFAFANUZI KUHUSU MSAMAHA WA KODI KWA WANAOANZA BIASHARA


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imeendelea kutoa ufafanuzi juu ya msamaha wa kodi kwa wale wanaoanza biashara.

Afisa msimamizi kodi mkuu  wa TRA makao makuu  Bw. Philipo Eliamini, ameimbia Shinyanga One Media kuwa, hatua hiyo imetokana na mabadiliko ya vipengere mbalimbali vya sheria ya kodi, ambayo yamekuja kufuatia mabadiliko ya sheria ya fedha ya mwaka 2026, yaliyopitishwa na Bunge kupitia bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2026/2027.

Kwa mujibu wa Afisa huyo wa TRA, mabadiliko hayo yamefanywa kwa lengo la kuwapa unafuu wananchi  wa kuanzisha biashara na kuwasaidia wafanyabiashara wadogo kukua kibiashara ili baadaye waje kuwa walipa kodi wazuri.

Akifafanua juu ya vigezo vya kupata msamaha huo umebainisha kuwa, walengwa ni wafanyabiashara wadogo wanaoanza biashara kwa mara ya kwanza, waliopata namba ya mlipa kodi  (TIN) ya biashara kwa mara ya kwanza na ambao mauzo yao  kwa mwaka  yaanaanzia Shilingi Milioni 4 hadi Milioni 200.

Amesema mfanyabiashara mwenye vigezo vilivyobainishwa anatakiwa kuwasilisha mwenyewe maombi ya kupewa msamaha TRA, na baade atapewa fomu maalum ambayo atajaza taarifa muhimu za biashara yake, ili aweze kufanyiwa tathmini.

Baada ya tathmini kufanyika na TRA kujiridhisha na taarifa alizoziweka, atapewa msamaha  wa kodi kwa muda wa miezi 12, ambapo baada ya kipindi hicho  kupita, ataendelea na utaratibu wa kawaida wa kodi.

Hata hivyo, kwa wale ambao mauzo yao yataendelea kuwa chini ya Shilingi Milioni 4 kwa mwaka hata baada ya muda wa miezi 12 kupita, amesema wataendelea na msamaha wa kodi kama Sheria ya kodi inavyoelekeza.

Bw. Eliamini ameeleza kuwa, utekelezaji wa sheria hiyo tayari umeanza kuanzia tarehe 1, Julai, 2026, na ametumia nafasi hiyo kuwahimiza wananchi kufungua na kusajili biashara zao, ili kunufaika na msamaha huo.


CHINI NI PICHA ZA MWONEKANO WA OFISI ZA TRA MKOA

 WA SHINYANGA

Post a Comment

0 Comments