Tukio hilo limetokea leo, Agosti 13, 2026, majira ya saa 11:45
asubuhi katika Kijiji na Kata ya Kisesa, Tarafa ya Sanjo, Wilaya ya Magu.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad
Mtafungwa, mwanafunzi wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Wita na mkazi
wa Kisesa, alikuwa akivuka barabara kutoka upande wa kulia kwenda kushoto
alipogongwa na lori hilo.
Kamanda Mtafungwa amesema lori lililohusika katika ajali
hiyo ni lenye namba za usajili T 885 ENK, aina ya Scania, mali ya
Kampuni ya Seedco Tanzania Limited, lililokuwa likisafiri kutoka Mwanza mjini
kuelekea Bariadi.
Amesema lori hilo lilikuwa likiendeshwa na Mdamo Nyalwisila
(40), mkazi wa Bariadi, ambaye tayari amekamatwa na anashikiliwa na Polisi kwa
ajili ya hatua zaidi za kisheria.
Kamanda Mtafungwa amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa
ajali hiyo ilisababishwa na uzembe wa dereva kushindwa kuchukua tahadhari
alipokuwa akiendesha katika eneo lenye makazi ya watu.
Kufuatia kifo hicho, wananchi waliokuwa eneo la tukio
walifunga barabara kuu ya Mwanza–Musoma na kuzuia magari kupita, wakitaka hatua
zichukuliwe dhidi ya dereva pamoja na kuwekwa hatua za kudhibiti mwendo wa
magari katika eneo hilo.
Viongozi mbalimbali wa Serikali walifika eneo la tukio na
kufanya mazungumzo na wananchi, huku wakiwaomba kuwa watulivu na kuacha vyombo
vya dola vichukue hatua kwa mujibu wa sheria.
Aidha, ombi la wananchi la kuwekwa matuta katika eneo hilo
lilikubaliwa, hatua inayolenga kupunguza mwendo wa magari na kuongeza usalama
kwa wakazi pamoja na watumiaji wengine wa barabara.
Hata hivyo, licha ya wito huo, baadhi ya wananchi walikaidi
na kuanza kurusha mawe, hali iliyosababisha Polisi kutumia mabomu ya machozi
kuwatawanya na kurejesha utulivu.
Kamanda Mtafungwa amewataka madereva kuwa makini na
kuzingatia taratibu za usalama wanapopita katika maeneo yenye makazi ya watu,
ikiwemo kupunguza mwendo na kufuata alama za barabarani.
Pia amewataka watembea kwa miguu na watumiaji wengine wa
barabara kuchukua tahadhari wanapovuka au kutumia barabara, huku wazazi
wakihimizwa kuwafuatilia na kuwaongoza watoto wadogo ili kuepusha ajali
zinazoweza kuzuilika.
(Chanzo IPP Media)

0 Comments