Mbunge wa Jimbo la Itwangi Azza Hillal Hamad, amesema
kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025/2030, vitongoji viwili
vya Kihongwe na Mizanza vilivyopo katika Kijiji cha Mwamanyuda Kata ya Imesela
wilayani Shinyanga, vitanufaika na mpango wa kusambaza umeme ngazi ya
vitongoji.
Azza amebainisha hayo wakati akizungumza na
wananchi katika mkutano wa hadhara wa kusikiliza kero zao na kuzitafutia
ufumbuzi.
Amesema, katika vitongoji hivyo viwili, Kitongoji cha
Kihongwe chenye kaya 157 na Kitongoji cha Mizanza chenye kaya 95, jumla
zinakuwa kaya 252 zitakazonufaika na huduma hiyo ya umeme katika kijiji cha
Mwamanyuda.
“Watu wa REA wameshafika na kufanya tathmini yao, na
kinachosubiriwa ni nguzo kupelekwa na kuanza kuwekewa umeme,” amesema Azza.
Aidha, amewataka wananchi kuanza kufanya “wiring” katika nyumba zao, na kuwa tayari kulipa Sh. 27,000 kwa ajili ya kuunganishiwa huduma hiyo kwenye kaya zao.
“Nawaomba wenyeviti wa vitongoji, kuna maeneo nimekutana na changamoto kwamba
wenyeviti wa vitongoji, mkikutana na watu wa REA, kuna maeneo mnaacha
kuwapitisha kwenye nyumba, na nguzo zinakwenda kupita mbungani kwa ajili ya
kufuata watu wawili au watatu na kuwaacha watu wengi “center”. naomba sana
msifanye makosa hayo,” amesema Azza.
Aidha, amesema ndani ya miezi hiyo sita pia barabara ya
Maskati–Ng’homango imeshachongwa imechongwa, ambapo awali miundombinu yake
ilikuwa mibovu, hasa wakati wa masika.
Katika mkutano huo, wananchi waliuliza maswali kuhusu kukamilika kwa jengo la zahanati, ukosefu wa umeme, uchakavu wa miundombinu ya shule ya msingi Kihongwe pamoja na ukosefu wa maji safi na salama.
SOURCE: Jamii focus










0 Comments